Social

Friday, February 10, 2017

Rais Kenyatta arekodi video na madansa Ikulu



Kwa ufupi
Rais huyo wa Kenya, Uhuru Kenyatta alirekodi video hiyo Jumatano akiwa na kundi hilo na anaonekana akijaribu kudansi sambamba na madansa hao wakati wakicheza wimbo wa “Bamba Kura Yako” unaohamasisha vijana kujiandikisha kupiga kura.

By Mwandishi Wetu, Mwananchi
Dar es Salaam. Rais amezua kizaazaa baada ya kurekodi video akicheza muziki na kundi la madansa la FBI akiwa Ikulu ya Nairobi, jambo lililosababisha wananchi wamshambulie kwenye mitandao ya kijamii.
Rais huyo wa Kenya, Uhuru Kenyatta alirekodi video hiyo Jumatano akiwa na kundi hilo na anaonekana akijaribu kudansi sambamba na madansa hao wakati wakicheza wimbo wa “Bamba Kura Yako” unaohamasisha vijana kujiandikisha kupiga kura.
Kenyatta anaonekana akiwa amevalia jaketi jekundu linalofanana na mavazi ya madansa hao, lakini likitofautiana kwa rangi.
Madansa hao wanaonekana wakiinamisha vichwa chini na kunyoosha mkono mmoja pembeni na mwingine ukiwa umekunjwa sambamba na kichwa, mithili ya mtu anayelia akiwa amejifunika uso.
Lakini wananchi walihamaki kwenye mitandao ya kijamii wakimtaka aamke, wakitumia alama (hash tag) ya #DabOfShame kumkosoa kutokana na kutotatua mgogoro na madaktari ambao wamegoma tangu mwaka jana.
Madaktari walianza mgomo Desemba 5 mwaka jana wakitaka ongezeko la asilimia 300 la mishahara, kuangaliwa upya kwa mazingira ya kazi, mfumo wa kazi na vigezo vya kupandishwa cheo, na utatuzi wa tatizo la upungufu wa wafanyakazi katika hospitali za Serikali.
Mmoja wa wachangiaji kwenye mitandao ya kijamiii aliyejitambulisha kwa jina la Juma, aliliambia gazeti la Star kuwa Kenyatta anajishughuli zaidi kupiga danadana madai ya madaktari.
Wauguzi wa Kenya hawaelewi inakuwaje rais aweze kudansi wakati wagonjwa wakihangaika na wengine kufariki.
“(Serikali) Inawaambia wagonjwa waende kujiandikisha wakati hospitalia hazifanyi kazi...nani amewaroga Wakenya,” alihoji Geoffrey Osiba akiongea na gazeti la Star.

Wengine walisema Kenyatta amechoka na hana budi kuruhusiwa kupumzika mwezi Agosti.

0 comments:

Post a Comment