By Cledo Michael, Mwananchi
mwananchipapers@mwananchi.co.tz
Dar es
Salaam. Kitendo cha Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu kuchukua fomu ya
kuwania urais ndani ya Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) na angalizo la
Rais John Magufuli kwamba taasisi hiyo ya kitaaluma isigeuzwe kuwa ya kisiasa,
kimeufanya uchaguzi wa viongozi wa wanasheria hao mwezi ujao kuwa na msisimko
wa aina yake.
Baada ya
kauli hiyo ya Rais Magufuli ambayo ilifuatiwa na ile ya Waziri wa Katiba na
Sheria, Dk Harrison Mwakyembe ya kutishia kukifuta chama hicho kama
kitajihusisha na masuala ya kisiasa, wanasheria na wanasiasa walijitokeza
kupinga wakiitaka Serikali isiingilie uchaguzi huo.
Misuguano
hiyo imewafanya si wanasheria, wasomi na wadau wa masuala ya sheria pekee,
kufuatilia kinachoendelea ndani ya TLS na uchaguzi huo, bali wananchi kwa
ujumla hivyo kuufanya kuwa na msisimko mkubwa tofauti na mwingine wowote uliowahi
kufanyika pengine tangu kilipoanzishwa mwaka 1954.
Kabla ya
Rais kutoa angalizo hilo, mchakato wa uchaguzi huo ikiwamo waliochukua fomu
haukuwa umewekwa wazi lakini baada ya ‘kuzinduliwa’ ufuatiliaji ulikuwa mkubwa
hasa baada ya kamati ya uchaguzi ya TLS kupitisha majina matano ya wanaowania
urais.
Mbali ya
Lissu ambaye pia ni Mbunge wa Singida Mashariki, wengine waliojitokeza kugombea
nafasi hiyo ni kada wa Chadema ambaye kabla ya kujiunga na chama hicho alikuwa
Mbunge wa Nyamagana (CCM) na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Lawrence Masha.
Pia yumo aliyewahi kuwa Rais wa TLS katika ya mwaka 2011 hadi 2013, Francis
Stolla, Godwin Mwapongo na Victoria Mandari.
Uchaguzi
wa TLS unatarajiwa kufanyika Machi 18 na mawakili 6,000 watapiga kura na
kumpata mrithi wa Rais wa sasa John Seka.
Awali,
Lissu alisema ameamua kuwania nafasi hiyo kutokana na Rais Magufuli kusema kuna
kampeni zinazoendeshwa na chama fulani (hakukitaja) kwenye uchaguzi huo wa TLS.
Pia, Lissu
alisema kauli ya Rais ya kwamba mawakili wanaowatetea wauza dawa za kulevya
wakamatwe imemfanya agombee ili kulinda Katiba na sheria za nchi.
Hata
hivyo, alipoulizwa kuhusu mrengo wake wa kisiasa, Lissu alisema masuala ya
kisheria hayana uhusiano na vyama vya siasa na kwamba jukumu la chama hicho ni
kulinda katiba na sheria.
“Sigombei
ili kupeleka Chadema ndani ya TLS. Masuala haya yanatuhusu sisi wote kujua
mambo yanapoharibika, kuona sheria zinapokiukwa na kuona sheria mbovu
zinapotungwa,” alisema alipohojiwa na mwandishi wetu.
Upepo huo
ulibadilika zaidi baada ya Dk Mwakyembe kutoa tishio la kuifungia TLS ikiwa
itajihusisha na siasa.
Dk
Mwakyembe katika tamko lake ambalo wadadisi wa masuala ya kisiasa wanadai
kwamba lililenga kukionya chama hicho kuhusu wagombea ambao pia ni wanasiasa,
alisema ikiwa kimeamua kubadili mwelekeo, kiende kwa Msajili wa Vyama Siasa ili
kisajiliwe rasmi la sivyo atapeleka bungeni mapendekezo ya kufuta sheria
iliyokianzisha.
Kauli hiyo
mbali ya kupingwa vikali ndani ya nchi, hivi karibuni, Chama cha Wanasheria
Afrika Mashariki (EALS) kilimwandikia barua Dk Mwakyembe kikimtaka aache
kuingilia uchaguzi huo kwani kufanya hivyo ni kuvunja sheria.
Barua hiyo
ambayo iliandikwa na Rais wa EALS, Richard Mugisha ilisema TLS si chama cha
kisiasa na kimeanzishwa kwa kufuata taratibu zote.
Maoni ya
wanasheria
Alipoulizwa
maoni yake kuhusu uchaguzi huo, Wakili wa kujitegemea, Methew Kakamba alisema
umekuwa gumzo kutokana na kauli za baadhi ya wagombea akiwamo Lissu aliyedai
kuwa ameamua kuwania nafasi hiyo kutokana na kile alichokisema Rais Magufuli
juu ya TLS.
“Lissu
siyo mwanasheria tu, ni mbunge sasa anapotamka kauli zinazomtaja mkuu wa nchi
(Rais), watu wanafuatilia kwa ukaribu zaidi,” alisema akizungumzia sababu za
uchaguzi wa mwaka huu ndani ya chama hicho kuwa na msisimko mkubwa zaidi.
Alisema
itikadi za chama hazimfanyi mtu kukosa vigezo kwa kuwa ni haki yake kikatiba na
kwamba hata yeye ni kada wa CCM licha ya kuwa wakili hivyo demokrasia inabidi
ifuatwe.
Mwanasheria
mwingine, Thomas Msasa alisema baada ya wagombea ambao ni maarufu na nguli
katika siasa kugombea, kumeongeza hamasa zaidi tofauti na ilivyokuwa katika
uchaguzi uliopita.
“Katiba
inatupa uhuru, uchaguzi ufanyike kwa haki bila kujali vyama. Tunahitaji Rais
ambaye anaweza kutetea masilahi ya mawakili na siyo ya vyama vya siasa wala
matakwa yake,” alisema Msasa.
Wakili
Josephat Kasegero alisema uchaguzi wa mwaka huu umeonekana kuwa na mvuto
kutokana na jinsi Lissu anavyopambana na Serikali katika masuala mbalimbali
akisema yumkini hiyo ndiyo sababu ya Rais Magufuli na Dk Mwakyembe kutoa
matamko hayo.
“Lissu ni
mwanasheria wa kawaida lakini kwa wakati huu ameonekana akipambana sana na
kuipinga Serikali ndiyo maana inakuwa hivyo,” alisema Kasegero.
Alisema
katika kinyang’anyiro hicho mwanasiasa si Lissu pekee, bali yuko Masha na
wanaompinga wanadhani kwamba anaweza kuingiza siasa kwenye chama cha kitaaluma.
Kampeni
zaendelea
Wakati
danadana hizo za kisheria na kisiasa zikitawala kuelekea uchaguzi huo, kampeni
za kuwania nafasi hiyo zinaendelea licha ya kwamba hakuna utaratibu maalumu wa
uratibu.
Ofisa
Maboresho ya Sheria wa TLS, Mackphason Buberwa alisema hadi sasa hakuna
mabadiliko wala malalamiko yaliyowasilishwa kwa chama hicho na kampeni
zinaendelea kama kawaida.
“Sisi kama
sekretarieti hatuhusiki na kupanga utaratibu lakini kuna majukwaani wanayotumia
kuendesha shughuli hizo,” alisema.
0 comments:
Post a Comment