Social

Monday, February 27, 2017

Jinsi Mbowe, Wema Sepetu walivyobadili upepo



By Bakari Kiango, Mwananchi bkiango@mwananchi.co.tz
Dar es Salaam. Wakati Mwenyekiti wa Chadema Freeman Mbowe akikumbwa na misukosuko baada ya kukamatwa na polisi wiki hii, kuliibuka jambo jingine jipya.
Miss Tanzania 2006 na msanii wa filamu nchini, Wema Sepetu alibadili upepo wa siasa nchini kwa kutangaza kuihama CCM na kuhamia Chadema jambo ambalo limejadiliwa na wasomi na wachambuzi wa siasa kwa mitazamo tofauti.
Ilianza kwa mwanasheria wa Chadema, Tundu Lindu kujitokeza mahakamani kumtetea Wema Sepetu katika kesi ya kudaiwa kukutwa na bangi. Lilionekana ni jambo la kawaida.
Lakini, kitendo cha Wema kumsindikiza Mbowe mahakamani kikashtua wengi.
Na hata alipotangaza kuhamia chama hicho cha upinzani pamoja na mama yake, mjadala ukawa mkubwa zaidi katika vijiwe, sehemu za starehe na mitandao ya kijamii.
Wakati mijadala hiyo ikiendelea, Wema akiwa na viongozi hao wa Chadema walikuwa miongoni mwa mashabiki waliojitokeza kushuhudia mechi ya watani wa jadi, wakati Simba ilipoifunga Yanga mabao 2-1 katika Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam jana.
Hali ilivyokuwa
Mbowe atakuwa anamaliza mapumziko ya mwishoni mwa wiki, akitafakari msukosuko uliohusisha kukamatwa na vyombo vya dola na kufikishwa mahakamani, lakini akijiliwaza baada ya chama chake kupata mwanachama mpya mwenye umaarufu mkubwa nchini, Wema Sepetu.
Kiongozi huyo wa Kambi ya Upinzani Bungeni alitakiwa kuripoti kituo kikuu cha polisi cha Dar es Salaam tangu Februari 10, lakini akakaidi, akisema kuna taratibu za kuita watu polisi na hivyo kuendelea na shughuli za Bunge mjini Dodoma hadi lilipomalizika.
Mbowe ni miongoni mwa watu 65 waliotajwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda ambaye aliwataka waripoti kituo hicho cha polisi kwa ajili ya mahojiano kuhusu biashara na matumizi ya dawa za kulevya.
Orodha ya watu hao inahusisha pia wafanyabiashara, wasanii na viongozi wa dini.
Lakini, kamanda wa polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Simon Sirro alisisitiza wito wa Mbowe kuripoti polisi, akisema walijaribu kumtafuta kwa njia ya simu hakupatikana na wala hawakuweza kumpata nyumbani kwake.
Kamishna Sirro alitoa saa 48 kwa Mbowe awe ameripoti polisi na asipofanya hivyo, atatafutwa kwa namna ambayo jeshi hilo litaona inafaa.
Siku moja kabla ya Mbowe kukamatwa, Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu aliliambia gazeti hili kuwa ingekuwa ni kumshauri, angemwambia asiripoti polisi hadi taratibu zitakapofuatwa.
Baada ya kurudi jijini Dar es Salaam, Mbowe alikamatwa Jumatatu wiki hii na kupelekwa kituo kikuu cha polisi ambako alihojiwa na pia kupelekwa nyumbani kwake kupekuliwa na kuachiwa saa 7:00 usiku, kwa mujibu wa mwanasheria wa Chadema, Tundu Lissu.
Taarifa za Mbowe kuwa polisi zilikuwa za aina tofauti; viongozi wa Chadema wakisema mwenyekiti wao alijipeleka kituoni wakati polisi ilisema ilimkamata.
Ofisa Habari wa Chadema, Tumaini Makene alisema mwenyekiti huyo alikuwa katika gari akitoka nyumbani kwake Kawe, ndipo alipokutana na gari la polisi na kutakiwa kusimama.
Baadaye, Wakili wa mwenyekiti huyo, Frederick Kihwelo aliyekuwa naye siku hiyo, alisema baada ya kutoka kituoni hapo polisi wapatao 10 walikwenda kufanya upekuzi nyumbani kwa kiongozi huyo.
Hatua ya Mbowe kukamatwa ilisababisha Edward Lowassa (waziri mkuu wa zamani na mjumbe wa kamati kuu wa Chadema), kukatiza mapumziko yake mkoani Arusha na kurejea Dar es Salaam.
Siku iliyofuata, Mbowe alilazimika kwenda Mahakama Kuu ambako amefungua kesi dhidi ya Makonda, Sirro na Mkuu wa Upelelezi wa Kanda ya Maalumu ya Dar es Salaam(ZCO), Camillius Wambura.
Katika kesi hiyo, Mbowe anapinga mamlaka yao ya kuamuru kukamatwa kwa wananchi na kuwekwa mbaroni huku akikitaka chombo hicho cha sheria kutamka Sheria ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa inayowapa mamlaka hayo kuwa ni batili kwa kuwa mazingira yaliyofanya iundwe, hayapo tena.
Mbowe alifungua kesi hiyo namba 01/2017 baada ya Makonda kumtaka aripoti polisi kwa mahojiano kuhusu biashara ya dawa za kulevya na matumizi.
Katika kesi hiyo, Mbowe pia aliiomba Mahakama Kuu itoe amri ya muda ya kuzuia polisi kumkamata na kumuweka mbaroni hadi shauri kuu litakapotolewa uamuzi.
Hali ilianza kubadilika Alhamisi wakati Mbowe alipokwenda Mahakamu Kuu kuendelea na kesi hiyo, akitegemea uamuzi kuhusu maombi yake ya kupewa kinga ya muda. Siku hiyo, Mbowe alienda mahakamani akisindikizwa na msanii nyota wa filamu, Wema Sepetu.
Kitendo cha Wema kumsindikiza kiongozi huyo wa upinzani kilibadili mwelekeo wa suala hilo, kutokana na macho ya wengi kuelekea kwa mshindi huyo wa taji la Miss Tanzania la mwaka 2006 ambaye katika kampeni za Uchaguzi Mkuu mwaka juzi alizunguka kushawishi vijana kuipigia kura CCM.
Siku hiyo, Serikali iliwasilisha pingamizi dhidi ya ombi la Mbowe la kutaka kinga ya muda ya kukamatwa na polisi na hivyo Mahakama Kuu kuamua kuwa uamuzi wa suala hilo utatolewa machi 2.
Picha za Wema akiwa na Mbowe mahakamani zilisambaa kwa haraka kwenye mitandao ya kijamii. Wema anaonekana kwenye picha hizo akiwa anatabasamu huku akiwa amenyoosha vidole viwili na vingine kuvikunja, ikiwa ni ishara ya Chadema, na pembeni yake akiwepo Mbowe, mbunge wa Bunda Ester Bulaya na mama wa msanii huyo.
Wakati Mbowe akienda mahakamani, ofisa uhusiano wa Chadema, Boniface Makene alitoa taarifa kwa vyombo vya habari akisema Wema ameamua kujiunga na chama hicho na kwamba angekabidhiwa kadi siku iliyofuata.
Badala yake, Wema, ambaye ni mtoto wa marehemu Balozi Isaack Sepetu, alitangaza uamuzi huo akiwa nyumbani kwao Mwananyamala, akisema ameamua “kuvaa gwanda” kwa hiari yake, hasa kwa kuwa ni mwanademokrasia.
Wema alisema kuna watu wengi nyuma yake, huku mama yake akisema ndugu zake wote wameamua kuihama CCM na kujiunga na Chadema.
Wasomi wamjadili Wema
Akizungumzia hatua hiyo ya Wema, Mhadhiri wa Sayansi ya Siasa wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT), Salim Hamad alisema huo ni mchezo wa siasa utakaoiathiri CCM.
“Safari ya Wema itakuwa na athari kwa kutegemea jinsi kila chama kinavyocheza karata yake ya mwisho,” alisema.
“Wema kama msanii ana wafuasi wengi pamoja na wasanii wenzake wenye ushawishi mkubwa. Athari yake pia itategemea jinsi wasanii wenzake watakavyomuunga mkono.
“Ulimwengu mzima, vyama vya siasa vinategemea celebrities (watu maarufu) kujitangaza. Zamani vyama viliandaa makada kwa kuwapa mafunzo na kuunda vikundi vilivyohamasisha. Siku hizi wasanii ndiyo wanategemewa kutangaza vyama vya siasa.”
Maoni ya Hamad yanalingana na mhadhiri mwingine wa sayansi ya siasa wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Richard Mbunda.
“Kwa sasa unaweza usione athari kubwa, lakini kwa kuwa Wema ni msanii mwenye wafuasi wengi hasa vijana na wao ndiyo wapiga kura, atakuwa na athari kwa CCM,” alisema Mbunda.
“Ukitaka kujua umuhimu wa Wema katika siasa ni pale CCM wenyewe walipomtumia kwenye kampeni za uchaguzi za mwaka 2015 kwa Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan. Hatuwezi kuona sasa kwa sababu si wakati wa uchaguzi, lakini kuna athari kubwa kisiasa.”
Hata hivyo, wasomi hao wanatofautiana na mchambuzi wa masuala ya siasa na jamii, Bubelwa Kaiza aliyesema kuondoka kwa Wema CCM kunaweza kuwa ni kujisafisha na tuhuma za kutumia dawa za kulevya.
“Chadema inajijengea taswira kwamba viongozi na wanachama wake wananyanyaswa katika vita ya dawa za kulevya, kwa hiyo watu kama Wema wataona kuwa huko ni sehemu ya kujioshea dhambi zao,” alisema Kaiza.
Kada wa Chadema na mchambuzi wa masuala ya siasa, uchumi na jamii, Albanie Marcosy alimzungumzia Wema kuwa miongoni mwa vijana walimbwende na wanapiganaji aliyejiweka wazi kushiriki na kupambania siasa ambaye atarudisha vijana waliowapoteza wakati wa uchaguzi.

“Ni kati ya watu waliofanikiwa kuwavuta nyuma vijana na hasa wasichana na kuacha kuunga mkono Chadema na tukapoteza sana ushawishi kwao,” alisema.

0 comments:

Post a Comment