Social

Monday, February 27, 2017

Steve Nyerere awapigia magoti JPM, Samia, Nape, Mwigulu sakata la Wema



By Elizabeth Edward, Mwananchi eedward@mwananchi.co.tz
Dar es Salaam. Siku chache baada ya sauti ya msanii wa filamu, Steve Nyerere kusambaa kwenye mitandao ya kijamii akisikika akizungumza na Mariam, ambaye ni mama mzazi wa Wema Sepetu, mwigizaji huyo wa sauti za viongozi, amejitokeza na kuwaomba radhi viongozi wote aliowataja.
Viongozi hao ni Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye na Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba. Wengine ni wabunge, Freeman Mbowe, Joseph Msukuma, Zitto Kabwe na Halima Bulembo.
Katika mazungumzo hayo yaliyorekodiwa pasi na yeye kujua, Nyerere anasikika akieleza jitihada alizofanya kuwashawishi wabunge na mawaziri kumsaidia Wema aliposhikiliwa na Polisi kutokana na tuhuma za kutumia dawa za kulevya.
Alisikika akisema baada ya Wema kukamatwa aliweka kambi bungeni Dodoma na kuwashawishi wabunge kuanzisha mjadala wa kumnasua katika sakata hilo.
Akizungumza na vyombo vya habari Dar es Salaam jana, msanii huyo alikiri kuwa sauti hiyo ni yake na kwamba alitoa kauli hizo kumridhisha mama Wema ambaye alikuwa akimlaumu kwa kushindwa kumsaidia bintiye licha ya ukaribu walionao.
“Naomba ukweli usipindishwe sauti ile ni yangu, maneno yale yalikuwa ya uongo niliyatoa kumtuliza mama na kujaribu kumzuia Wema asiondoke CCM maana walishaanza kusema akitoka ndani wanahamia Chadema.
Namuomba radhi Rais (John) Magufuli kwa kuwahusisha katika suala hili mawaziri wake aliowaamini na kuwateua kwenye nafasi nyeti, nilifanya hivyo kwa kulinda heshima ya chama changu maana sikuwa na namna ya kufanya kama binadamu.”
Alisema hana mpango wa kukihama chama hicho tawala na ataendelea kukipigania kwani ndicho ambacho kimemkuza.
Kuhusu madai ya kuwashawishi wabunge wajadili suala la Wema bungeni Nyerere alisema, “Namuomba radhi Spika kwa kusema niliwashinikiza wabunge kwa kuwa sina uwezo, ujanja wala mamlaka hayo, nilisema uongo.”
Alikanusha pia kuwa amevunja uhusiano na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda baada ya kutokea kwa sakata hilo kama alivyosikika kwenye sauti na kudai kuwa hana tatizo lolote na kiongozi huyo.
“Nje ya kazi yake Makonda ni ndugu yangu, siwezi kugombana naye tunazungumza vizuri kabisa, niko naye bega kwa bega na ninaunga mkono jitihada zake za kupambana na dawa za kulevya.”
Wasanii kuidai CCM
Nyerere ambaye alikuwa mwenyekiti wa wasanii walioshiriki kwenye kampeni za CCM na kaulimbiu yao ya “Mama Ongea na Mwanao” alisema hakuna hata mmoja ambaye hakulipwa kama inavyodaiwa.
Juzi, wakati akitangaza uamuzi wake wa kuhamia Chadema, Wema alisema yeye na wenzake wanadai fedha zao CCM na kila wanapofuatilia wamekuwa wakizungushwa na kuambiwa wamfuate Rais mstaafu Jakaya Kikwete.
“Kama yupo msanii ambaye alikuwa kwenye timu ya Mama Ongea na Mwanao na anaidai CCM ajitokeze, mimi nilikuwa mwenyekiti, wote tulilipwa inavyostahili, tena Wema ndiye anayeongoza kwa kulipwa vizuri akiwa kama Makamu Mwenyekiti,” alisema Nyerere.
Wakati akiendelea na mazungumzo hayo, msanii huyo alidondosha machozi huku akimtupia lawama Mama Wema kwa kitendo cha kumrekodi na kusambaza mazungumzo yao. “Hadi sasa najiuliza kwanini nirekodiwe? Mama hakuwa na nia njema na mimi. Je, ningeongea matusi mle ingekuwaje? Nimepata uchungu sana maana niliamini nilikuwa naongea na mama yangu ndiyo maana nikajiachia.

Jina hili nimelitafuta kwa miaka 25, halafu leo mama anakuja kunichafua, napitia kipindi kigumu mno lakini namwachia Mungu kwa kuwa nilifanya yote hayo kwa kumkumbatia Wema, malipo yake ndiyo haya.”

0 comments:

Post a Comment