By Kelvin Matandiko na Jesse Mikofu,
Mwananchi mwananchipapers@mwananchi.co.tz
Dar/Mwanza.
Hatua ya Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) kutoa orodha ya wanafunzi zaidi ya
8,000 ikisema taarifa zao za uhakiki zina kasoro hivyo kuwa hatarini kukosa
sifa za kuendelea na masomo, uongozi wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine
(Saut) kimesema baadhi ya walioorodheshwa walishamaliza masomo zaidi ya miaka
mitatu iliyopita.
Mbali na
kauli hiyo, chuo hicho, vyuo vingine vya elimu ya juu na wadau wa elimu
wameijia juu TCU wakisema taasisi hiyo ndiyo inayopaswa kubeba lawama.
Juzi, TCU
ilitoa orodha ya vyuo 52 ambavyo ilidai wanafunzi wake walidahiliwa katika
masomo ambayo hawakustahili na kutoa muda hadi Februari 28 kufanya uhakiki
vinginevyo watapoteza sifa za uanafunzi.
Lakini
jana, uongozi wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine ulisema Serikali ndiyo
inayopaswa kuwajibika.
Makamu
Mkuu wa Saut ambacho kimetajwa kuwa na wanafunzi 1,046 wasiokidhi vigezo, Dk
Thadeus Mkamwa alisema kuwa chuo hicho kilifuata taratibu zote lakini
wameshangaa TCU ambayo ndiyo yenye mamlaka ya kudahili wanafunzi, kutoa taarifa
zenye mkanganyiko.
Alikosoa
uhakiki huo wa TCU akisema wanafunzi waliotajwa katika chuo hicho, zaidi ya
asilimia 70 walihitimu masomo zaidi ya miaka miwili hadi mitatu iliyopita.
Alisema takribani mwezi mmoja uliopita, TCU ilitoa barua chuoni hapo ikieleza
kuwapo wanafunzi ambao vigezo vyao vina shaka na hasa namba ya utambulisho
(index number), hususani kwa wanafunzi wanaotoka nje ya nchi.
“Kigezo
kingine ni kwamba baadhi yao vyeti vya diploma havionekani lakini, wao ndiyo
wanaidhinisha, sasa tunajiuliza kazi yao ni ipi, haya ya kujitokeza mwishoni
wakati watu wameshahitimu? TCU ndiyo wenye mamlaka ya kudahili wanafunzi sisi
tunapokea tu majina ambayo wanaidhinisha, hata hizo namba za utambulisho wao
ndiyo wamepewa mamlaka kuzihakiki wala si vyuo husika.”
Dk Mkamwa
alisema iwapo kuna mabadiliko yanayofanywa bora taratibu zifuatwe kuliko kuleta
mkanganyiko unaosababishwa na ukiukwaji wa sheria na taratibu katika sekta hiyo
muhimu.
Makamu
Mkuu wa Chuo Kikuu cha Tumaini Dar es Salaam (Tudarco), Dk Joyce Chonjo alisema
wamepokea majina hayo na baada ya kukamilisha uhakiki, watazungumza.
Naibu
Makamu Mkuu wa UDSM, Profesa Florens Luoga alisema inawezekana kuna taarifa za
wanafunzi wao ambazo hazikukamilika kutokana na mazingira ya udahili wao.
Kwa mujibu
wa TCU, kuna wanafunzi 224 wa chuo hicho ambao uhakiki wao una kasoro.
“Kwanza,
sisi tunataka kujua TCU walichukua taarifa zipi, tunachotakiwa kufanya ni
kuwasaidia kukamilisha taarifa ili tuone orodha hiyo usahihi wake ni upi, kama
wapo hapa lazima tuwaondoe lakini lazima kufuata taratibu kwa usahihi na haki,”
alisema Profesa Luoga na kuongeza kuwa zaidi ya asilimia 50 ya wanafunzi hao
waliotajwa na TCU wanatoka Msumbiji.
0 comments:
Post a Comment