Social

Wednesday, March 1, 2017

Vigogo Quality Group wapanda kizimbani



By Cledo Michael na Taus Ally mwananchipapers@mwananchi.co.tz
Dar es Salaam. Wakati Mwenyekiti wa Kampuni ya Quality Group, Yusuf Manji akipata matibabu chini ya ulinzi wa polisi katika Hospitali ya Aga Khan, Meneja Mradi wa kampuni hiyo na katibu wake jana walifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.
Washtakiwa hao, Jose Kiran (Meneja Mradi) na Prakash Bhatt (Katibu), walipandishwa kizimbani wakikabiliwa na shtaka la kukiuka amri ya ofisa wa uhamiaji na kujaribu kutoroka.
Walisomewa mashtaka hayo mbele ya Hakimu Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Cpyrian Mkeha.
Mwendesha Mashtaka wa Uhamiaji, Method Kagoma akiwasomea mashtaka, alidai kuwa Februari 20, washtakiwa wakiwa ni raia wa India na waajiriwa wa Quality Group Ltd, walimzuia ofisa wa uhamiaji kufanya kazi zake.
Alidai kuwa, watuhumiwa walikataa kuripoti katika ofisi za uhamiaji zilizopo jijini Dar es Salaam na kujaribu kutoroka nchini kupitia Mpaka wa Horohoro.
Washtakiwa walikana kutenda kosa hilo na wako nje kwa dhamana baada ya kukamilisha masharti yaliyomtaka kila mmoja kuwa na mdhamini mmoja ambaye alisaini bondi ya Sh5 milioni. Kesi hiyo imeahirishwa hadi Machi 7, kwa ajili ya usikilizwaji wa awali pamoja na kuunganishwa na kesi ya washtakiwa wenzao 14.
Wakati huo huo; Mfanyabiashara Manji anaendelea kupatiwa matibabu katika Hospitali ya Aga Khan.
Awali Manji alilazwa katika Taaasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) Muhimbili, alikofikishwa baada ya hali yake kudhoofika alipokuwa ameshikiliwa katika Kituo Kikuu cha Polisi kwa tuhuma zilizohusu matumizi ya dawa za kulevya.
Mwandishi wa gazeti hili alifika hospitalini hapo jana saa 4:12 asubuhi ili kujua hali ya mfanyabiashara huyo.
Alimshuhudia Manji akiwa hospitalini hapo huku polisi mmoja akiwa eneo hilo.
Baada ya kufika mapokezi, mwandishi alimueleza mhudumu wa zamu kuwa alifika kutaka kujua hali ya Manji, lakini alimjibu kuwa hafahamu chochote na badala yake alimtaka aende kwa askari wa ulinzi ili ampe maelekezo. Hata hivyo, askari huyo alitoa maelekezo kuwa amuone mtu mwingine aliyekuwa jirani yake akiwa kavalia suti, kuwa ndiye mwenye majibu ya maswali yake.
Hata hivyo, kabla ya kumfikia mtu huyo, askari huyo alimuita tena mwandishi na kumtaka akazungumze na daktari anayemtibu Manji. Kabla ya mwandishi hajaanza safari ya kwenda kumuona daktari huyo, Manji alifika mapokezi akitokea wodini na kumtaka muuguzi amtolea nakala ya karatasi aliyokuwa ameishika mkononi. Kabla muuguzi hajafanya hivyo, alifika mwanaume mmoja mweusi na alimtaka Manji arejee wodini.

Msemaji wa hospitali hiyo, Olayce Lotha alipoulizwa kuhusu hali ya Manji, alisema mfanyabiashara huyo ametaka uongozi wa hospitali kutotoa taarifa zake kwa vyombo vya habari au mtu yeyote nje ya familia yake.

0 comments:

Post a Comment