Dar es Salaam. Siku moja kabla ya kuanza utekelezaji wa katazo la
pombe kali ndani ya vifungashio vya plastiki maarufu viroba, Kampuni ya Perfect
Printers Ltd, inayohusika na usambazaji wa vifungashio hivyo imeeleza kupata
hasara ya Dola za Marekani 65,000 sawa na Sh140 milioni.
Mkurugenzi mtendaji wa kampuni hiyo,
Perfect Lyimo akizungumza na gazeti hili jana alisema hasara hiyo inatokana na
tani 100 zilizotengenezwa na kulipiwa ambazo ni oda ya kampuni inayozalisha vinywaji
aina ya pombe kali.
Hatua hiyo ni utekelezaji wa agizo
lililotolewa Februari 18, na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa alipohutubia wakazi
wa Mji Mdogo wa Mirerani wilayani Simanjiro, akisema biashara hiyo ukomo wake
utakuwa Machi Mosi.
Katika ufafanuzi wake, Majaliwa alisema
tayari wamekaa na wenye viwanda na kukubaliana wanaotengeza pombe hizo waziweke
kwenye ukubwa unaokubalika.
Hata hivyo, Lyimo aliliambia gazeti
hili jana kuwa tani hizo zinatokea Durban, Afrika Kusini ambako zinazalishwa.
“Kwanza kuna tani 25 ambazo zinatakiwa kufika Dar es Salaam Machi 6, kutokea
Afrika Kusini. Mzigo mwingine ni kontena la tani 25 tunategemea ndani ya wiki
tatu zijazo utaletwa,” alisema na kuongeza:
“Pamoja na mzigo huo, pia kuna tani 50
ambazo zimeshatengenezwa na tumeshalipia tayari, zote tumeshalipia dola 65,000
hizo ni gharama za ununuzi na usafirishaji tu nje ya kodi na tozo za upakuaji
na upakiaji wa mzigo bandarini.”
Lyimo alisema hakuna namna yoyote ya
kuokoa hasara hiyo hadi sasa, kwani huandaa vifungashio kulingana na oda ya
kampuni inayozalisha ‘viroba’. Alisema pamoja na hasara hiyo, Serikali itakosa
VAT na tozo nyingine za upakuaji bandarini. Alifafanua akisema kampuni
iliyowaagiza mzigo huo haitaweza kupokea tena kutokana na katazo hilo la
Serikali na hakuna mbadala wa matumizi ya vifungashio hivyo ili kuokoa hasara
itakayotokea.
Mkurugenzi wa Sera na Ushawishi wa
Shirikisho la Wenye Viwanda nchini (CTI), Hussein Kamote akizungumza na gazeti
hili alisema Serikali ilitakiwa kuanza na utoaji adhabu kwa wafanyabiashara
wanaouza viroba hivyo kama njugu mtaani kwa kuwa ni kinyume cha sheria.
Alisema taratibu zinaeleza viroba hivyo
vinatakiwa kuuzwa katika maduka na maeneo maalumu ya starehe yenye leseni.
0 comments:
Post a Comment