Rais wa Marekani Donald Trump alifichua taarifa zinazofaa kuwa siri kuu kuhusu kundi linalojiita Islamic State (IS) kwa waziri wa mambo ya nje wa urusi, vyombo vya habari nchini Marekani vinasema.
Taarifa hizo, zilihusu kutumiwa kwa laptopu kwenye ndege, na zilitoka kwa mshirika wa Marekani ambaye hakuwa ametoa idhini kwa habari hizo kukabidhiwa Urusi, gazeti la Washington Post linasema.
Bw Trump alikutana na Sergei Lavrov katika afisi yake wiki iliyopita.
Mshauri mkuu wa usalama wa taifa wa Marekani HR McMaster amepuuzilia mbali madai hayo kwenye vyombo vya habari na kusema ni ya "uongo".
Tuhuma kwamba huenda maafisa wa kampeni wa Bw Trump waliwasiliana na maafisa wa Urusi zimegubika utawala wa rais huyo, na kufikia sasa uchunguzi unaendelea.
Lakini rais amepuuzilia mbali tuhuma hizo na kusema ni "habari za uongo".
Wakati wa kampeni, Bw Trump alimkosoa sana mpinzani wake wa chama cha Democratic Hillary Clinton, kwa jinsi alivyoshughulikia taarifa ambazo zinafaa kuwa siri kuu.
Nini hasa kilitokea?
Katika mazungumzo yake na Bw Lavrov pamoja na balozi wa Urusi nchini Marekani katika afisi yake White House, trump alifichua maelezo ambayo huenda yakapelekea kutambuliwa kwa mdokezi aliyetoa habari hizo, maafisa waliambia Washington Post na New York Times.
Walizungumzia njama ya IS. Rais huyo inadaiwa alianza kuzungumzia mambo ambayo alikuwa hajapangiwa kuyazungumza, na kufichua maelezo zaidi kuhusu njama hiyo.
Njama hiyo inadaiwa kujumuisha kutumiwa kwa laptop kwenye ndege. Mazungumzo ya trump yaligusia ni jiji gani kulikuwa kumegunduliwa tishio.
Habari hizo za kijasusi zilitoka kwa mshirika wa Marekani na zilichukuliwa kuwa za usiri mkubwa kiasi kwamba hazikufaa kufahamishwa washirika wengine wa Marekani, magazeti hayo yameripoti.
Wengine waliokuwepo katika mkutano huo waligundua kosa hilo la Bw Trump na wakachukua hatua kujaribu kuzima moto huo kwa kuwafahamisha maafisa wa CIA na maafisa wa Shirika la Usalama wa taifa (NSA), gazeti la Washington Post linasema.

Hatua ya Bw Trump si kwamba ni kinyume cha sheria, kwani Rais wa Marekani ana uhuru wa kuamua ni habari gani zitaorodheshwa kama siri kuu na gani hazitaorodheshwa kama siri kuu.
Mkutano huo ulitokea siku moja baada ya Bw trump kumfuta kazi mkuu wa FBI James Comey, hatua iliyoshutumiwa vikali kwamba FBI walikuwa tayari wanachunguza uhusiano wa maafisa wa kampeni wa Bw Trump na maafisa wa Urusi.
White House wamesema nini?
Mshauri mkuu wa usalama wa taifa HR McMaster ameambia wanahabari kwamba taarifa hizo, kama zilivyoripotiwa na magazeti hayo mawili, ni za uongo.
"Rais na waziri huyo wa mambo ya nje walizungumza kuhusu hatari mbalimbali zinazokabili nchi hizi mbili, zikiwemo hatari katika sekta ya uchukuzi wa kutumia ndege,2 alisema.
"Haikutokea - hata wakati mmoja - ambapo duru za kijasusi au njia za kupokea habari zilizungumziwa. Na rais hakufichua shughuli zozote za kijeshi ambazo kufikia sasa hazifahamiki na umma."
Kupitia taarifa, Waziri wa Mambo ya nje wa Marekani Rex Tillerson alikariri hilo na kusema maelezo ya ndani kuhusu "hatari mbalimbali" hayakuzungumziwa na kwamba wadokezi, njia au operesheni za kijeshi havikujadiliwa.
Gazeti la Washington Post, ambalo lilichapisha habari hizo kwanza, lilisema hilo si kukanusha taarifa hizo.

Mwanahabari Greg Jaffe aliambia BBC kwamba gazeti la Post liliweka wazi kwamba rais hakuzungumzia wadokezi wala njia za kupata habari hizo za kijasusi.
Lakini akaongeza: "Taarifa yetu ilizungumzia habari zenyewe ambazo zingewezesha Warusi kurudi nyuma na kufuatilia na kuweza kujua wadokezi na njia zenyewe. Alisema mengi sana kiasi kwamba wanaweza kujua hayo (mdokezi na njia hizo)."
0 comments:
Post a Comment